Thursday, November 26, 2009

TANZIA!

Mlemavu wa Ngozi Mariam Obed (18), amefariki Dunia juzi nyumbani kwao Eneo la Nkhungu Mjini kutokana na kuugua kansa ya Jicho kwa muda mrefu.
Nawashukuru sana wote waliojitolea kwa hali na mali kumsaidia mariam ili aweze kutibiwa, ndugu zangu waliomsaidia mariam HINAI TAMIM na SAID wote wa nchini Oman Muscat, mungu awazidishie baraka muendelee na moyo huo.
Mungu ailaze mahali Pema Peponi roho ya Mariam Obed

AMEN!!

Monday, September 21, 2009

MAPENZI hayana umri jamani, hebu msome mzee wa miaka 70 aliyejinyonga kwa wivu wa mapenzi!

Na Martha Mtangoo, Dodoma

9/21/2009

MZEE wa miaka 70 aliyefahamika kwa jina la Msuliche Mhogo amejinyonga kwa kutumia kamba kutokana na wivu wa mapenzi.

Kamnda wa polisi mkoani hapa Zelothe Steven aliwaambia waandishi wa habari ofisini kwake jana kuwa tukio hilo lilitokea juzi saa 2.30 asubuhi katika kijiji cha Ngh’ambi wilayani Mpwapwa.

Akielezea tukio hilo Kamanda Zelothe alisema kuwa chanzo cha mzee huyo kujinyonga ni kutokana na wivu wa kimapenzi kwa mkewe mwenye umri wa miaka (30) ambaye jina lake limehifadhiwa.

Alifafanua kuwa kwa muda mrefu mzee huyo alikuwa akihisi mkewe ana uhusiano wa kimapenzi na mwanaume mwingine hapo kijijini ambaye ni jirani yake.

Alisema kuwa awali kabla ya tukio hilo kutokea , usiku mzee huyo aligombana na mkewe kuhusu mtoto wao mmoja ambaye ana umri wa miaka miwili akidai kuwa mtoto huyo ni wa mwanaume ambaye nahisi anatembea naye na si mwanaye.

Kamanda Zelothe alisema kuwa wakati wakiendelea na ugomvi huo mke mkubwa wa mzee huyo alienda kuamua ugomvi huo na ilipofika asubuhi mzee huyo aliaga kuwa anaenda safari na ndipo alipokwenda kwenye mbuyu ambao upo jirani na nyumbani kwake na kujinyonga.

Wakati huohuo jeshi la polisi mkoani hapa linamshikilia Hamis Salum (27) mkazi wa Manispaa ya Moshi kwa tuhuma za kufungua duka na kuiba simu 10 za aina mbalimbali.

Kamanda Zelothe alisema kuwa baada ya kufungua mlango mtuhumiwa huyo alijfungia ndani ya duka hilo na kuanza kukusanya simu dukani humo ambapo mwenye duka ambaye ni Freeman Narcis (23) alifika dukani hapo na alipofungua duka alimkuta mtuhumiwa huyo akiendelea kukusanya vitu katika duka hilo .

Kamanda Zelothe alisema kuwa jeshi hilo bado linamshikilia mtu huyo kwa mahojiano zaidi na atafikishwa mahakamni mara baada ya uchunguzi kukamilika.

Ends……

Thursday, August 20, 2009

Ningekuwa Spika Sitta Ningejiuzulu!


NINGEKUWA SPIKA SITTA NINGEJIUZULU

HAKI ya Mungu kweli duniani kuna mambo pamoja na mambo yote mazuri ambayo spika wa Bunge la Jamhuri ya muungano wa Tanzania Samuel Sitta kwa Wabunge wa chama cha mapinduzi wakiwemo na Mafisadi ambao wanajulikana kwa majina mimi sitaki kuwataja bado wabunge hao ambao wengine ni wajumbe wa halmashauri kuu ya chama cha mapinduzi (NEC) na mafisadi wamo wamememgeuka!

Jamani kwa kweli ni lazima tukajifunza ustaarabu mengi sita kawasaidia wabunge hawa pamoja na wale wa upinzani lakini sasa tena moto umemgeukia yeye jamani kweli hii ni fair?
Hapa naorodhesha tu mambo machache ambayo spika sitta amewapigania wabunge hawa na kubalansi Bunge ili liliemee upande mmoja halafu akaonekana kana kwamba anapendelea upande mmoja wa CCM!

Spika huyuhuyu ambaye anaitwa Mbabe amepigania kwa nguvu marupurupu ya wabunge na kusababisha sasa hivi wabunge kulipwa mshahara tu kiasi cha sh. Milioni 12 kwa mwezi na marupurupu kibao!

Hiyo haikutosha spika huyohuyo mbabe amepigania mpaka sheria ya kuanzishwa mfuko wa maendeleo ya Jimbo kwa wabunge umepita kwa mbinde Bungeni licha ya wananchi kuonyesha kuukataa!

Mimi sijatumwa na Mtu kuzungumzia hili suala ila nimeguswa na kitendo alichofanyiwa hivi karibuni Mjini Dodoma katika Ukumbi wa Nec wa kutaka avuliwe uanachama kwa kuwa anaendesha eti Bunge kibabe!

Kwa kweli CCM hamkumfanyia Spika wenu sawa kabisa kwa sababu mnataka aliendesheje Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambalo hivi sasa limekuwa kama Kikundi cha vichekesho cha orijino Komedi kuna jambo lingine zaidi ya hili si mseme?

Alichokisema hivi karibuni Bungeni spika kuwa anaomba ulinzi wa ziada kwa kuwa nguvu ya mafisadi inamzidi alikuwa sahihi kwa kuwa tayati alishaona nini kinafuata na kwa kuwa serikali haikumuelewa ndiyo maana ilipuuzia na maneno meengi ya kejeli yakatolewa juu ya kauli yake!

Lakini ukweli wa maneno ya Mzee Sitta sasa yamejidhihirisha ndani ya mkutano wa CCM ambamo kunaonekana kuwa CCM bila mafisadi haiwezekani kuwa hai, sasa mnataka spika aendesheje Bunge lenu JAMANI?

Mnataka spika atoe uhai wake ndiyo mbaini kuwa alikuwa anaendesha bunge kwa usawa na kubalansi pia au mnatakaje au aendeshe Bunge kwa kupendelea wabunge wa CCM? Mtalishusha hadhi na viwango pia kama mnataka liwe ambavyo ninyi mnataka liwe!
Kwa hali hii mimi ningekuwa Spika Sitta ningejiuzulu Uspika ili kuwaachia nafasi mafisadi kumtafuta spika ambaye wao wanamtaka ambaye hatendesha Bunge kibabe au sio na kupendelea CCM maana viwango ulivyoahidi mwaka ule havitakuwepo tena!

Kwa kweli inauma halafu inakera zaidi inatia kichefuchefu kufanya hivyo ni kuonyesha ni kiasi gani kwamba CCM inashikiliwa na kuendeshwa na watu wachache wenye pesa zao na utartibu huu ambao CCM mmeuonyesha sijui nini kitafuata lakini mmetia DOA tena doa lenyewe jekundu kwenye nguo nyeupe!

SHAURI YENU CCM angalieni msije mkajuta kwa kuwasafisha watu ambao tayari walishachafuka siku nyingi kupitia watu ambao wangekusaidieni kuwasafisha angalau kwa kutumia busara zao ambazo zinaonekana ni ubabe!



Tuesday, June 23, 2009

Wasamalia wema wamsaidia Binti Mariam




Picha kushoto; Mwandishi na mmiliki wa Blog hii Martha Mtangoo, akimkabidhi fedha taslim sh. 230,00 Mariam ambaye alikuwa akihitaji msaada kwa ajili ya kufanyiwa operesheni ya saratani ya Jicho ambayo tayari ameshafanyiwa, fedha hizo
ambazo zimetolewa na wasamalia wema Hinai Tamim na Said ambao wanaishi nchini Oman.
Mungu awabariki sana.

Tuesday, May 05, 2009

WENZETU HUKO TARIME wanadumisha mila kwa mtindo huu

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI LAWRANCE MASHA
AMA kweli ukistaajabu ya Mussa uyaona ya Firauni! wakati watu wanapinga mila na desturi zilizopitwa na wakati huko TARIME wenzetu wanadumisha tu!
hebu soma hii kwanza.

Katika mkoa wa Mara kuna mila ambayo imekuwa ikifanywa na wazee wa kimila ambao kutokana na kutekeleza mila hizo matukio ya mauaji yamekuwa yakisababishwa na mapigano ya koo mbalimbali.
Mila hiyo imesababisha hali ya ulinzi na usalama mkoa ni mara kutokuwa shwari na kutoridhisha kutokana na matukio ya mara kwa mara ya mauaji ya kiukoo, wizi wa mifugo, ujambazi wa kutumia silaha na biashara ya madawa ya kuelevya hususan kilimo cha Bangi.
Wazee wa Kimila Mkoani Mara ndiyo viongozi na waamrishaji wa mapigano ya koo yanayondelea, ambapo wazee hao hunufaika na mapigano hayo kwa kupata mgao wa mali zilizoporwa katika mapigano.
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Lawrance Masha anasema kuwa mila na desturi za baadhi ya makabila zinachochechea mapigano baina ya vijana wa koo moja na koo nyingine vitendo ambavyo vimekuwa vikiheshimika miongoni mwa jamii hizo kuwa ni vya kishujaa.
Waziri Masha anasema kuwa wazee wa kimila wamekuwa viongozi na waamrishaji wa mapiganmo hayo ambapo wamekuwa na maradaka makubwa katika Koo zao na hutoa adhabu kali kwa vijana wanaokwepa kushiriki mapigano.
Waziri Masha anasema kuwa kutokana na hilo, hadi sasa hali ya ulinzi na usalama katika mkoa wa Mara si ya kuridhisha kwa kuwa kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya mauaji ya kiukoo, wizi wa mifugo, ujambazi wa kutumia silaha na biashara ya madawa ya kulevya hususan kilimo cha bangi.
Anasema kuwa matukio hayo yameenea katika wilaya za Tarime, Rorya na wilaya ya Musoma vijijini ambapo koo za hunyaga na Wamera na koo za Waanchari na Warenchoka na Wakira na Wanyabasi na Wairegi zimekuwa zikipigana mara kwa mara.
Masha anasema kuwa kilimo cha Bangi ambacho kimekuwa ni chanzo kikubwa cha uchumi kwa baadhi ya makabila katika mkoa wa Mara, pia kimekuwa ni chanzo cha mapigano hayo ambapo imekuwa ni kawaida kwa watu katika maeneo hayo kukodishwa na wakala kulima bangi na kulipwa fedha nyingi.
Anasema kuwa pale inapotokea kuwa mkulima wa Bangi aliyekodishwa hakufanikiwa kuvuna Bangi kutokana na Bangi hiyo kuharibika kutokana na ukame au kuharibiwa na vyombo vya dola, mkulima huyo hutakiwa kurudisha fedha alizopewa na wakala wake ambapo ili kupata fedha ya kurudisha, mkulima huiba ng’ombe za koo jirani na kuuza.
Waziri huyo anasema kutokana na mapigano hayo jumla ya watu 136 walifariki na zaidi ya 336 walijeruhiwa huku nyumba 2421 zikichomwa moto na kuacha zaidi ya kaya 756 zikiwa hazina mahali pa kuishi na vihenge 673 vya kuhifadhia mahindi kuchomwa moto katika kipindi cha kuanzia mwaka 2001 hadi machi mwaka huu.
Anazitaja hatua ambazo serikali imeshazichukua kuwa ni pamoja na kuifanya wilaya za Tarime na Rorya kuwa mkoa wa Kipolisi ili kukabiliana ipasavyo na matishio ya usalama, uhalifu na wahalifu.
Hatua nyingine ambayo Waziri Masha anaitaja kuwa ni ile ya serikali ya mkoa kupitia Tawala za mikoa na Serikali za mitaa (TAMISEMI), kufanya kampeni mbalimbali kwa kushirikiana na taasisi nyingine zikiwemo za dini, wanasiasa, wizara ya elimu na kushawishi wananchi kuachana na mapigano. Waziri Masha anasema kuwa mikutano ya ujirani mwema baina ya Vyombo vya dola vya Tanzania na Kenya inaendelea kufanyika ili kuimarisha mahusiano miongoni mwao, ambapo mapema mwezi.

HAYA AKINA MURA KAZI KWENU BWANA, IRA MUBADIRIKE ETI!

Tuesday, April 21, 2009

JAMANI, Ndugu zangu mnaombwa kumsaidia huyu mpendwa Anaumwa!


MLEMAVU wa ngozi Mariamu Obedi (18)mkazi wa eneo la Nkhungu mjini Dodoma ameiomba Serikali pamoja na wanachi wamsaidie fedha kwaajili ya matibabu ya kansa ya jicho ili aweze kwenda hospitali ya Ocean Road ya jijini Dar-es-Salaam kutibiwa.

Ombi hilo alilitoa jana wakati alipokuwa akizungumza na mmiliki wa blog hii mjini Dodoma huku akilia kutokana na maumivu makali anayoyapata yanayosababishwa na uvimbe uliopo katika jicho lake la kushoto kuuma.

Alikielezea kuanza kuugua jicho hilo alisema kuwa kilitokea kiupele kidogo katika jicho hilo na hivyo kuanza kuvimba ikiwa ni pamoja na kumsababishia maumivu makali.

Mariamu alisema kuwa baada yakuona hali hiyo ikizidi kuendelea aliamua kwenda katika hospitali kuu ya Mkoa wa Dodoma kwaajili yakupata matibabu.

Mlemavu huyo wa ngozi (albino) alifafanua kuwa alianza kuumwa mwaka 2007 ambapo alipoenda katika hospitali hiyo ya mkoa wa Dodoma uongozi wa hospitali hiyo ulimwandikia barua aende hospitali ya Mvumi.

Alisema kuwa baada ya kwenda katika hospitali hiyo ya Mvumi pia walishindwa kumtibia na hivyo kumuandikia barua wakimtaka aende jijini Dar-es-Salaam katika hospitali ya Msasani ambapo alikwenda na kufanyiwa oparesheni na kupata nafuu.

Alibainisha kuwa baada ya kupata naafuu alirejea tena Dodoma anapoishi ambapo alikaa kwa muda wa mwaka mmoja ambapo ni 2008 na ilipofika mwaka huu hali hiyo ilimrudia tena na hivyo kulazimika kurudi tena katika hospitali kuu ya mkoa wa Dodoma.

Mariamu anafafanua kuwa alipofika katika hospitali hiyo alipimwa na hivyo kuonekana kuwa ana ugonjwa wa kansa ambapo anatakiwa kwenda hospitali ya Ocean road kutibiwa.

Hata hivyo ameiomba Serikali na watu wenye mapenzi mema ambao wataguswa na tatizo alinilonalo, kumsaidia chakula kutokana na mama yake mzazi Cahrerine Peter kutokuwa na uwezo hali ambayo inamsababisha kulala njaa licha ya yeye kunywa dawa kali na hivyo kumfanya kukosa nguvu kutokana na kukosa chakula.

KAMA UMEGUSWA KUMSAIDIA BINTI HUYU, TAFADHALI WASILIANA KUPITIA NAMBA HII' +255713358273, AU tumia akaunti hii 029201039794, NBC Bank Mazengo Branch.

Mungu akubariki sana.